Iringa. Mwenyekiti wa Tume
Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele,
amewataka wasimamizi wa uchaguzi nchini kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sheria za uchaguzi na kanuni zake,
akisisitiza kuwa hawapaswi kufanya kazi kwa mazoea bali kwa kufuata maelekezo
ya Tume.
Jaji Mwambegele ametoa wito huo
Januari 24, 2026 mkoani Iringa wakati akifungua mafunzo ya siku tatu kwa
waratibu wa uchaguzi wa mikoa, wasimamizi wa uchaguzi, wasimamizi wasaidizi
ngazi ya jimbo na kata, maafisa uchaguzi, maafisa ununuzi pamoja na wahasibu.
Mafunzo hayo yanafanyika kuanzia Januari 24 hadi 26, 2026.
Akizungumza katika hafla hiyo,
amewapongeza wajumbe wa Tume pamoja na waratibu wa uchaguzi wa Mikoa ya Songwe
na Ruvuma kwa uteuzi wao, akisema umezingatia weledi, haki, uwazi na matakwa ya
Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani.
Amesema matarajio ya Tume ni
kuona chaguzi zinaendeshwa kwa uadilifu wa hali ya juu, huku akisisitiza
umuhimu wa wasimamizi wa uchaguzi kuheshimu viapo walivyoapa na kuzingatia
maelekezo yote yatakayotolewa na Tume.
“Msifanye kazi kwa mazoea. Kila
uchaguzi una mazingira na changamoto zake tofauti,” amesisitiza Jaji
Mwambegele.
Aidha, amewataka wasimamizi wa
uchaguzi kuvishirikisha vyama vyote vya siasa vyenye usajili kamili pamoja na
wadau wengine wa uchaguzi katika masuala muhimu ya kiuchaguzi. Pia amesisitiza
umuhimu wa kuyafahamu vizuri maeneo yatakayohusika na uchaguzi, ikiwemo
miundombinu ya kufikia vituo vya kupigia kura.
Mafunzo hayo yamelenga kuwajengea
uwezo wasimamizi wa uchaguzi ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi,
hususan katika Uchaguzi Mdogo wa Ubunge Jimbo la Peramiho na Uchaguzi wa Diwani
Kata ya Shiwinga, Mkoa wa Songwe.
Uchaguzi huo umeitishwa kufuatia
vifo vya Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Jenista Muhagama, na Diwani wa Kata ya
Shiwinga, Lusekelo Mwalukomo.
Kwa upande wake, Mratibu wa
Uchaguzi Mkoa wa Ruvuma, Athumani Kateula, amewahimiza wananchi wenye sifa
katika Jimbo la Peramiho kujitokeza kuchukua fomu za kugombea nafasi ya ubunge,
kushiriki kikamilifu katika kampeni na hatimaye kujitokeza siku ya uchaguzi
kuchagua kiongozi mwenye sifa.
Naye Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo
la Mbozi, Danny Tweve, amesema maandalizi ya Uchaguzi wa Diwani Kata ya
Shiwinga yanaendelea vizuri, akibainisha kuwa wamejipanga kuhakikisha hatua
zote za uchaguzi—kuanzia uteuzi wa wagombea, kampeni hadi siku ya kupiga kura—zinasimamiwa
kwa kuzingatia Katiba na sheria za nchi.
Kabla ya kufunguliwa rasmi kwa
mafunzo hayo, wasimamizi wa uchaguzi walikula kiapo cha kujitoa katika
uanachama wa vyama vya siasa, hatua iliyolenga kuimarisha misingi ya uwazi,
haki na kutokuegemea upande wowote katika usimamizi wa chaguzi.





Comments