
Iringa. Halmashauri ya Manispaa
ya Iringa imeshauriwa kusimamia kikamilifu ukusanyaji wa mapato yatokanayo na
vibali vya ujenzi ili kuongeza mapato na kuwezesha utekelezaji wa miradi ya
maendeleo.
Ushauri huo umetolewa leo na
Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Sifaeli Kivamba, wakati wa mkutano wa
Baraza la Madiwani kwa kipindi cha robo ya pili ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Kivamba alisema halmashauri
inapoteza mapato kutokana na kutosimamia ipasavyo utoaji na matumizi ya vibali
vya ujenzi, huku ujenzi ukiendelea katika maeneo mbalimbali bila vibali halali.
“Kuna ujenzi unaendelea kila siku
lakini wengi hawana vibali, hali ambayo inainyima Serikali mapato. Naomba
waheshimiwa madiwani mfuatilie suala hili katika maeneo yenu kwa kuhoji kila
anayeendelea na ujenzi kama ana kibali,” alisema Kivamba.
Hata hivyo, aliipongeza Baraza la
Madiwani kwa kusimamia vyema muda wa mkutano huo uliodumu kwa saa moja na nusu
pekee, ikilinganishwa na awali ambapo vikao vilikuwa vikichukua hadi saa sita.
Alisema hali hiyo imetokana na mafunzo (semina) waliyopewa madiwani kuhusu
uendeshaji wa vikao pamoja na matumizi ya vishikwambi (tablets).
Kwa upande wake, Meya wa Manispaa
ya Iringa, Ibrahim Ngwada, aliwataka wafanyabiashara ndogondogo wanaofanya
biashara katika maeneo yasiyo rasmi kuondoka mara moja na kuelekea katika
maeneo waliopangiwa ili kuweka mji katika mpangilio mzuri na kulinda mazingira.
Ngwada alisema hayo leo wakati
akijibu swali la Diwani wa Viti Maalum Kanda ya Mlandege, Husna Mtasiwa, katika
kipindi cha maswali na majibu, akisisitiza kuwa wafanyabiashara hao
hawaruhusiwi kufanya biashara barabarani au maeneo mengine yasiyo rasmi.
Awali, Mtasiwa alihoji ni lini
halmashauri itawawezesha wafanyabiashara hao kuhamia katika maeneo rasmi baada
ya kuondolewa katika maeneo yasiyoruhusiwa.
Naye Diwani wa Kata ya Mlandege,
Wakili Dickson Chaula, aliuliza ni lini halmashauri itaboresha mazingira ya
ukusanyaji mapato katika Soko la Kisasa la Mlandege maarufu Soko la Mwamwindi.
Akijibu swali hilo, Mkurugenzi wa
Manispaa ya Iringa ambaye pia ni Katibu wa Baraza, Zaina Mlawa, alisema
Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya ukusanyaji mapato kwa kuwataka
wafanyabiashara wote waliopo sokoni hapo kuzingatia mikataba yao ili kuwezesha
ukusanyaji wa mapato kwa ufanisi kwa maendeleo ya manispaa.




Comments