Iringa. Mwenyekiti wa Wazazi Wenye Watoto Wenye Ulemavu Mkoa wa Iringa, Bw. Zawadi Msigalla, amesema ana ndoto ya siku moja kuwa Mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kuwatetea watu wenye ulemavu na makundi maalum, akimuomba Rais Samia Suluhu Hassan amkumbuke katika nafasi 10 za uteuzi wa wabunge.
Bw. Msigalla, ambaye ni mtu mwenye ulemavu, amesema dhamira yake ya kuingia bungeni inatokana na uzoefu wake wa muda mrefu katika utetezi wa haki za watoto wenye ulemavu na wazazi wao, akibainisha kuwa sauti ya kundi hilo bado haijapewa uzito unaostahili katika vyombo vya maamuzi.
“Nina ndoto ya kuwa Mbunge ili niweze kuzungumza kwa niaba ya wazazi na watoto wenye ulemavu. Tuna changamoto nyingi zinazohitaji uwakilishi wa moja kwa moja,” amesema Msigalla.
Akizungumza na Pamlomo- Sauti Ya Jamii mesema anaamini kuwa kupitia nafasi za uteuzi wa Rais, bado kuna fursa kwa watu wenye ulemavu na watetezi wao kushiriki kikamilifu katika kutunga na kusimamia sheria.
Mbali na kuwa mwenyekiti wa wazazi hao, Msigalla pia ni Afisa Mhamasishaji wa shirika lisilo la kiserikali la Kiitaliano la Nyumba Ali, linalojihusisha na miradi ya kijamii ikiwemo elimu jumuishi, afya na ustawi wa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.
Kupitia nafasi hiyo, amesema amekuwa akihamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kuwajumuisha watoto wenye ulemavu katika shule za kawaida, kupambana na unyanyapaa na kuhakikisha wanapata huduma stahiki za afya na kijamii.
Msigalla amesema iwapo atapata uteuzi, atapigania kuimarishwa kwa sera na sheria zinazolinda haki za watu wenye ulemavu, kuongeza bajeti kwa ajili ya elimu jumuishi pamoja na kuboresha upatikanaji wa huduma za tiba na vifaa saidizi.
“Watu wenye ulemavu wana uwezo mkubwa. Tunachohitaji ni kuaminiwa na kupewa nafasi. Nikiingia bungeni, nitakuwa sauti ya wale ambao mara nyingi hawasikiki,” amesema.
Alizaliwa mwaka 1998 wilayani Tunduru, mkoani Ruvuma, kabla ya kuhamia Iringa alipokutana na shirika la Nyumba Ali lililomsaidia katika masomo yake. Amesema alikumbana na changamoto nyingi za kukataliwa na shule kutokana na ulemavu wake.
“Nimesoma kwa msaada wa shirika la Nyumba Ali. Bila wao nisingeweza kusoma kwa sababu baadhi ya shule zilinikataa kutokana na hali yangu,” amesema.
Msigalla alihitimu mwaka 2022 katika Chuo Kikuu cha Kikatoliki Ruaha (RUCU) aliposomea sheria ngazi ya cheti, na baadaye kuajiriwa na shirika hilo kama Afisa Mhamasishaji.
Akizungumzia maisha yake binafsi, amesema ndoa yake na mkewe, Atupenda Valentino Ng’ande, imekuwa ushuhuda kwamba watu wenye ulemavu wanaweza kuishi maisha ya kawaida na yenye heshima kama wengine.
Kwa upande wake, Bi. Ng’ande amesema licha ya changamoto za maneno kutoka kwa baadhi ya watu, ameamua kusimama imara na kuonesha kuwa ndoa yao imejengwa katika upendo na heshima.
Baadhi ya wazazi wa watoto wenye ulemavu mkoani Iringa wameeleza kumuunga mkono Msigalla, wakisema uzoefu wake wa moja kwa moja katika kukabiliana na changamoto za malezi na utetezi unamfanya kuwa kiongozi anayeelewa mahitaji halisi ya kundi hilo.
Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais ana mamlaka ya kuteua wabunge 10 kwa lengo la kuongeza uwakilishi wa makundi mbalimbali bungeni.
Msigalla anaamini kuwa uteuzi wa mtu mwenye ulemavu au mtetezi wao utakuwa ishara ya kuimarisha usawa na ujumuishaji katika uongozi wa kitaifa.



Comments