Na Mwandishi Wetu
Mafinga. Mbunge wa Mafinga Mjini,
Dickson Lutevele maarufu kama ‘Villa’, akishirikiana na Mbunge wa Viti Maalumu
– Mwakilishi wa Vijana, Jasmin N'gumbi, amewataka vijana wanaofanya shughuli
katika Stendi ya Mabasi Mafinga kuimarisha umoja wao ili waweze kunufaika na
fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali kwa kushirikiana na wadau wa
maendeleo.
Akizungumza na vijana hao,
Lutevele alisema mshikamano na umoja ni nguzo muhimu itakayowawezesha kupata
mikopo, mafunzo pamoja na mitaji kupitia mipango ya uwezeshaji wa vijana.
“Serikali imeweka mazingira
rafiki kwa vijana kujikwamua kiuchumi, lakini ni lazima muwe na umoja imara na
vikundi vinavyotambulika rasmi ili iwe rahisi kuwafikia na kuwasaidia,” alisema
Lutevele.
Kwa upande wake, N’gumbi
aliwahimiza vijana hao kufanya kazi kwa nidhamu na kujiepusha na vitendo
vinavyoweza kuharibu taswira ya eneo la stendi, akisisitiza kuwa umoja wao
utawapa sauti ya pamoja katika kudai na kupata haki zao.
Katika kuonesha dhamira ya
kuwasaidia, wabunge hao walichangia jumla ya Sh700,000 taslimu kwa vikundi
mbalimbali vinavyofanya shughuli katika eneo la stendi hiyo, fedha ambazo
zinalenga kuimarisha mfuko wa vijana na kusaidia shughuli zao za kila siku.
Vijana hao waliwashukuru viongozi
hao kwa mchango huo na kuahidi kuendeleza umoja pamoja na kutumia fedha hizo
kwa malengo yaliyokusudiwa.




Comments