Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, imemhukumu kifungo cha miaka miwili jela askari polisi, Sajenti Rogers Mmari, baada ya kupatikana na hatia ya kosa la kuua bila kukusudia katika tukio lililosababisha kifo cha Nashon Kiyeyeu (23).
Hukumu hiyo ilitolewa Machi 19, 2026 na Jaji Angaza Mwipopo,
kufuatia mahakama kuridhika na ushahidi wa upande wa mashtaka uliothibitisha
kuwa mshtakiwa alihusika na kifo cha Kiyeyeu, mkazi wa Nyamhanga, Manispaa ya
Iringa.
Katika kesi hiyo, ilielezwa kuwa tukio hilo lilitokea
Desemba 14, 2024 katika eneo la Ipogoro, ambapo marehemu alishambuliwa na
askari huyo kwa kushirikiana na mgambo, Thomas Mkembela, hali iliyosababisha
kupoteza maisha yake. Tukio hilo lilihusishwa na tuhuma za wizi wa simu ya
mkononi inayodaiwa kuwa ya Beatrice Baraka Kimata.
Akisoma hukumu, Jaji Mwipopo alisema ushahidi uliowasilishwa
haukuonesha kuwepo kwa nia ya moja kwa moja ya kuua, hivyo mahakama ikamtia
hatiani kwa kosa la kuua bila kukusudia chini ya vifungu namba 195 na 198 vya
Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16.
Mahakama ilibainisha kuwa marehemu alipata majeraha makubwa
mwilini, ikiwemo kupasuka kichwa na kuganda kwa damu kwenye ubongo, hali
iliyosababisha kifo chake. Aidha, ushahidi wa mazingira ulionyesha kuwa
marehemu alionekana mara ya mwisho akiwa na mshtakiwa ndani ya gari lake aina
ya Toyota Noah.
Ilielezwa pia kuwa baada ya tukio hilo, mshtakiwa
alikimbilia Moshi akidaiwa kufanya hivyo kwa lengo la kupoteza ushahidi, kabla
ya kukamatwa na kurejeshwa Iringa kwa ajili ya uchunguzi na hatua za kisheria.
Mahakama ilibaini pia kuwa hakukuwa na kumbukumbu yoyote ya mtuhumiwa katika
daftari la mahabusu (detention register) katika Kituo cha Polisi Ipogoro.
Katika utetezi wake, wakili Cleofas Mheluka aliiomba
mahakama kumpunguzia adhabu mshtakiwa, akieleza kuwa ni baba wa watoto watano,
ana matatizo ya kiafya ikiwemo shinikizo la damu (BP) na maumivu ya mgongo, na
kwamba hiyo ni mara yake ya kwanza kukabiliwa na kosa la jinai. Pia alidai kuwa
tukio hilo halikuwa la kukusudia.
Kwa upande wa familia ya marehemu, baba wa marehemu, Lusiani Kiyeyeu, alisema hajaridhishwa na hukumu hiyo, akidai kuwa adhabu iliyotolewa ni ndogo ukilinganisha na uzito wa tukio, na kuiomba serikali kuingilia kati ili haki itendeke kikamilifu.
Hukumu hiyo imeibua mjadala miongoni mwa wananchi, baadhi
wakidai adhabu hiyo ni ndogo, huku wengine wakisema ni fundisho kwa watumishi
wa umma kuhusu umuhimu wa kuwajibika katika utekelezaji wa majukumu yao.
Historia ya Tukio
Awali, Desemba 15, 2024, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa,
SACP Allan Bukumbi, aliwaeleza waandishi wa habari kuwa Sajenti Rogers alipokea
taarifa kutoka kwa mwananchi aliyemtuhumu Kiyeyeu kuiba simu.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, askari huyo kwa kushirikiana na
mgambo walimkamata mtuhumiwa na kumpiga, hali iliyosababisha kupoteza fahamu.
Baadaye walimpeleka katika hospitali binafsi na kisha Hospitali ya Rufaa ya
Mkoa wa Iringa, ambako ilibainika kuwa tayari amefariki dunia.
Kamanda Bukumbi alisema baada ya tukio hilo, watuhumiwa
walitoweka na kuanza kusakwa na jeshi la polisi, huku akitoa wito kwa yeyote
mwenye taarifa kusaidia ili sheria ichukue mkondo wake.


Comments