Mtoto huyo ambaye alikuwa
mwanafunzi wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Zizi, alikutwa akiwa
amefariki nje ya nyumba yao, tukio lililosababisha taharuki na huzuni kwa
wakazi wa eneo hilo.
Kwa mujibu wa majirani na ndugu
wa familia, mwili wa mtoto huyo uligunduliwa asubuhi ya Machi 7, 2026, nje ya
nyumba yao baada ya juhudi za kumtafuta kuanza kufanyika kufuatia kutoweka
tangu usiku.
Jirani wa familia hiyo, Jacob
Mwalongo, alisema walifanya jitihada za kumtafuta mtoto huyo bila mafanikio,
kabla ya kutoa taarifa katika kituo cha polisi.
“Tulianza kumtafuta huku na kule
lakini hatukumpata. Jioni tulikwenda kutoa taarifa polisi. Asubuhi tulipata
taarifa kutoka kwa jirani mmoja kuwa mtoto amepatikana akiwa ameanguka karibu
na nyumba. Tulipofika eneo hilo tulikuta tayari amefariki dunia ndipo
tukaripoti tena polisi,” alisema Mwalongo.
Jirani mwingine, Adela Issack,
alisema walipata taarifa za kupotea kwa mtoto huyo majira ya usiku na wakaanza
jitihada za kumtafuta, lakini hazikuzaa matunda.
“Baadaye asubuhi nilipigiwa simu
na kuambiwa mtoto amepatikana. Tulipofika eneo la tukio tulikuta mwili wake
umefunikwa kwa shuka,” alisema Issack.
Aliongeza kuwa walitoa taarifa
kwa askari wa polisi na viongozi wa usalama wa eneo hilo, ambapo uchunguzi wa
awali wa mwili ulibaini kuwa mtoto huyo alikuwa na majeraha ikiwemo kuvunjika
mkono na shingo kuonekana kulegea, kabla ya mwili kupelekwa katika chumba cha
kuhifadhia maiti kwa uchunguzi zaidi.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Njiapanda, Maisha
Modestus, alisema tukio hilo ni la kusikitisha na kwamba tayari taarifa
zimefikishwa kwa vyombo vya dola ili uchunguzi ufanyike na wahusika wachukuliwe
hatua za kisheria.
“Niwahakikishie wananchi kuwa
uongozi wa mtaa unaendelea kushirikiana na vyombo vya usalama ili kubaini
chanzo cha tukio hili na kuwabaini waliohusika,” alisema Modestus.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa,
SACP Allan Bukumbi, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa jeshi
la polisi linaendelea na uchunguzi ili kuwabaini na kuwakamata wote
waliohusika.
Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri
James, akiongozana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, alifika nyumbani kwa
wazazi wa marehemu kutoa pole kwa familia na kufuatilia tukio hilo.
RC James alieleza kuwa serikali
haitavumilia vitendo vya ukatili dhidi ya watoto na kuagiza Halmashauri ya
Manispaa ya Iringa kudhibiti mara moja uuzwaji wa pombe za kienyeji majumbani,
akisema tabia hiyo imekuwa ikichangia matukio ya uhalifu katika jamii.
Alisisitiza kuwa hatua kali
zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayebainika kuhusika na tukio hilo.






Comments