Iringa. Chuo Kikuu cha Ruaha Catholic University (RUCU)
mkoani Iringa kimezindua rasmi tovuti mpya ya kisasa iliyounganishwa na
teknolojia ya Akili Unde (Artificial Intelligence – AI) kwa lengo la
kurahisisha upatikanaji wa taarifa na huduma kwa wanafunzi, wazazi na wadau wa
elimu.
Akizindua tovuti hiyo Machi 11, 2026, Makamu Mkuu wa chuo
hicho, Profesa Chrispina Lekule, alisema RUCU kama taasisi ya elimu ya juu
inaendelea kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanayoendelea
duniani.
Alisema kupitia maboresho na tafiti mbalimbali, chuo
hicho kimefanikiwa kubuni tovuti ya kisasa yenye muundo unaorahisisha matumizi
kwa watumiaji kupitia simu za mkononi au kompyuta.
“Tovuti hii mpya (www.rucu.ac.tz) imeboreshwa kwa muundo wa kisasa
unaorahisisha matumizi kwa watumiaji kupitia simu au kompyuta. Pia
imeunganishwa na teknolojia inayomwezesha mtumiaji kuuliza maswali mbalimbali
kuhusu RUCU na kupata majibu sahihi papo hapo,” alisema Profesa Lekule.
Alifafanua kuwa teknolojia hiyo itasaidia kuongeza
ufanisi wa mawasiliano kati ya chuo na wadau wake pamoja na kuboresha utoaji wa
huduma kwa wanafunzi, wazazi na walezi.
Kupitia tovuti hiyo, watumiaji wataweza kupata taarifa
mbalimbali ikiwemo programu za masomo na ada zake, uongozi wa chuo, huduma za
wanafunzi pamoja na fursa za ushirikiano na uwezekano wa kupanga miadi na
viongozi wa chuo.
Aidha, tovuti hiyo pia itaunganisha wahitimu wa chuo
(alumni), kuonesha miradi mbalimbali inayotekelezwa na RUCU, machapisho ya
kitaaluma, shughuli za huduma kwa jamii pamoja na maisha ya wanafunzi chuoni
ikiwemo vipaji na bunifu zao.
Alisema tovuti hiyo itarahisisha upatikanaji wa taarifa
kwa haraka bila kulazimika kusafiri au kupiga simu.
“Katika dunia ya sasa, kuokoa muda na gharama ni jambo
muhimu. Badala ya mtu kusafiri kutoka mbali kuja Iringa kuuliza maswali,
anaweza kuuliza moja kwa moja kupitia tovuti na kupata majibu papo hapo,”
alisema Dk Migodela.
Aliongeza kuwa hata badala ya kupiga simu, mtu anaweza
kuuliza maswali mbalimbali kupitia tovuti hiyo na hivyo kuokoa gharama za
mawasiliano.
Naye Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa RUCU (RUCUSO), Mussa
Nelson Labia, alisema tovuti hiyo itasaidia kuitangaza RUCU ndani na nje ya
nchi pamoja na kuwawezesha wanafunzi kupata huduma mbalimbali kwa urahisi.






Comments