
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri
James, amesema ushiriki wa baba katika malezi na makuzi ya watoto ni muhimu
katika kujenga kizazi chenye maadili mema na uwezo wa kuchangia maendeleo ya
taifa, hatua inayosaidia kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya 2050.
RC James alitoa kauli hiyo wakati
akifungua mdahalo wa pamoja wa kujadili ajenda ya malezi uliofanyika katika
Chuo Kikuu Kishiriki cha Mkwawa (MUCE) mkoani Iringa, aliyoandaliwa na taasisi
ya Montessori Community of Tanzania (MCT) kwa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa
kupitia Idara ya Ustawi wa jamii mkoa.
Alisema baba ana nafasi kubwa
katika malezi ya watoto na kwamba ushiriki wake husaidia watoto kukua katika
mazingira ya upendo, ulinzi na maadili mema, hali inayochangia kujenga jamii
imara na yenye uwajibikaji.
“Malezi bora ya mtoto hayawezi
kufanywa na mzazi mmoja pekee. Ushirikiano wa baba na mama ni muhimu ili mtoto
akue katika mazingira yanayomjengea nidhamu, maadili na uwezo wa kuchangia
maendeleo ya taifa,” alisema RC James.
Ofisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa
Iringa Martin Chuwa alibainisha kuwa katika baadhi ya familia, baba wamekuwa
wakiachwa nyuma au kujiondoa katika majukumu ya malezi, jambo ambalo linaathiri
ukuaji na maendeleo ya watoto.
Alisisitiza umuhimu wa jamii
kuhamasisha ushiriki wa baba katika malezi ili kuhakikisha watoto wanapata
malezi bora yatakayowaandaa kuwa raia wema na wenye mchango katika maendeleo ya
nchi.
Mdahalo huo uliwakutanisha wadau
mbalimbali wakiwemo wasomi, wanafunzi na viongozi wa jamii kwa lengo la
kujadili namna bora ya kuimarisha malezi ya watoto na kuwajenga katika misingi
imara ya maadili na uwajibikaji.





Comments