Watoto mjini Iringa leo wameonekana kufurahia Sikukuu ya Idd Pili kwa kushiriki michezo mbalimbali katika eneo la Garden, ambapo wazazi na walezi waliwapeleka watoto wao kusherehekea siku hiyo kwa furaha na burudani.
Katika viwanja hivyo, watoto walishiriki michezo tofauti ikiwemo bembea, magari ya watoto na michezo mingine ya burudani, huku wengine wakionekana kufurahia vyakula na vinywaji vilivyokuwa vikiuzwa eneo hilo.
Baadhi ya wazazi walisema wameamua kuwapeleka watoto wao katika eneo hilo ili kuwapa nafasi ya kufurahia sikukuu hiyo na kujenga kumbukumbu nzuri za utotoni.
“Ni muhimu watoto wakapata muda wa kucheza na kufurahia sikukuu kama hii. Inawasaidia kuwa na furaha na pia kukuza mahusiano yao na wenzao,” alisema mmoja wa wazazi aliyekuwepo eneo hilo.
Aidha, wafanyabiashara waliokuwa eneo hilo walieleza kufurahishwa na ongezeko la wateja, wakisema siku hiyo imekuwa fursa nzuri kwao kuongeza kipato kupitia biashara ndogondogo.
Maadhimisho ya Idd Pili mjini Iringa yameendelea kwa amani, huku wananchi wakitumia siku hiyo kusherehekea pamoja na familia zao na kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii.
Comments