Na Friday Simbaya, Iringa
Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa limekamata jumla ya watuhumiwa 53 kwa makosa mbalimbali ya uhalifu katika operesheni zilizofanyika maeneo tofauti kuanzia Aprili Mosi, 2026, huku likitoa onyo kali kwa wananchi dhidi ya utoaji wa taarifa za uongo zinazosababisha taharuki.
Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, SACP Allan Bukumbi, alisema miongoni mwa waliokamatwa ni Ramadhani Mussa (33), dereva mkazi wa Dar es Salaam, aliyetiwa hatiani kwa kosa la kutoa taarifa za uongo kuwa ameibiwa sehemu zake za siri.
Kwa mujibu wa Bukumbi, mahakama ilimhukumu Mussa kifungo cha miaka mitano jela baada ya kuthibitika kuwa taarifa aliyotoa haikuwa ya kweli.
“Katika operesheni hizi, tumefanikiwa pia kuwakamata watu wengine waliokuwa wakitoa taarifa za uongo na kusababisha taharuki kwa wananchi,” alisema Bukumbi.
Aliwataja watuhumiwa wengine kuwa ni Mussa Kaundi (39), mfanyabiashara mkazi wa Mafinga, pamoja na wenzake wawili kutoka Isakalilo, Manispaa ya Iringa, na Usokami, Mafinga, ambao kwa nyakati tofauti walidai kuibiwa sehemu zao za siri.
Alieleza kuwa uchunguzi wa kitabibu ulithibitisha madai hayo hayakuwa ya kweli, huku upelelezi wa kesi hizo ukiwa umekamilika na watuhumiwa wakitarajiwa kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.
Katika hatua nyingine, Kamanda Bukumbi alisema Jeshi la Polisi linaendelea kutoa elimu kwa madereva wa vyombo vya moto na watumiaji wengine wa barabara kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani.
Alisema baadhi ya madereva wamechukuliwa hatua za kisheria kutokana na makosa ya barabarani, ikiwa ni pamoja na kufungiwa leseni.
Aliwataja madereva hao kuwa ni Efes Ndembela, aliyefungiwa leseni kwa miezi mitatu kuanzia Aprili 8, 2026, baada ya kukutwa akiendesha basi lenye namba T249 DYD aina ya Zhongtong, mali ya kampuni ya New Force Enterprises, kwa mwendo kasi katika eneo la Iyovi.
Mwingine ni Ally Mbwilo, aliyefungiwa leseni kwa miezi mitatu kuanzia Aprili 10, 2026, kwa kosa la kuendesha basi lenye namba T840 DUS aina ya Fuso, mali ya kampuni ya Alimwene, kwa mwendo kasi akiwa njiani kutoka Iringa kuelekea Ruaha Mbuyuni.
Jeshi la Polisi limetoa wito kwa wakazi wa Iringa na wananchi kwa ujumla kuacha kujihusisha na vitendo vya uhalifu na upotoshaji wa taarifa, na badala yake kushirikiana na vyombo vya dola ili kudhibiti vitendo hivyo mapema.
- Get link
- X
- Other Apps

Comments